1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wahanga wa Tigray wafungua kesi dhidi ya Ethiopia

Saumu Mwasimba
8 Februari 2022

Taasisi binafsi ya masuala ya kisheria imefungua kesi ya malalamiko dhidi ya Ethiopia katika Tume ya Haki za Binadamu na Haki za Wananchi ya Afrika.

https://p.dw.com/p/46gwT
Nord-Tigray Verletzte nach Luftangriffen
Picha: REUTERS

Taasisi hiyo  inayoitwa Legal Action Worldwide -LAW - inadai kuna ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu nchini humo dhidi ya raia katika eneo la kaskazini la Tigray.

Taasisi hiyo ya kisheria kupitia mawakili wake imesema inawawakilisha wahanga kutoka jimbo la Tigray ambao wametowa ushahidi wa kesi hiyo lakini hawawezi kuorodheshwa kama walalamikaji kutokana na hofu ya kuandamwa na serikali.

Taarifa iliyotolewa na mawakili wa taasisi hiyo imefahamisha kwamba Ethiopia inahusika na visa vingi vya ukiukaji wa haki za binaadamu chini ya mkataba wa sheria za Afrika ikiwemo hatua ya wanajeshi kuwalenga raia pamoja na miundo mbinu ya raia, mauaji ya watu wengi, unyanyasaji wa kingono,ukamataji wa watu bila makosa pamoja na kuwafunga watu. Hata hivyo, sio serikali ya Ethiopia  wala tume hiyo ya haki za binadamu na haki za wananchi yenye makao makuu yake nchini Gambia, iliyotowa tamko lolote kuhusu kesi hiyo.